Ni watu wachache sana ndiyo wanaopenda na wanafahamu umuhimu wa kusoma vitabu. Watu wengi hasa waafrika hawapendi kusoma vitabu ikiwa hakuna kinachowalazimisha kufanya hivyo kama vile mtihani, kazi, n.k.
Kwa hakika kuna maarifa mengi yaliyofichwa kwenye vitabu; hii ndiyo sababu watu wengi waliofanikiwa husoma au hata kuandika vitabu.
Ikiwa unataka kupata maarifa na kuboresha maisha yako kwa njia ya kusoma vitabu, basi fahamu faida 15 za kusoma vitabu.
1. Hukuongezea marifa mapya
Lengo kubwa linalowafanya waandishi wa vitabu kuandika vitabu ni kuweka maarifa yao kwenye maandishi. Hivyo kwa kusoma vitabu unapata maarifa mbalimbali yaliyowekwa kwenye kitabu husika.
Hivi leo kuna vitabu vinavyohusu takriban kila kitu; kwa hiyo maarifa yoyote unayoyahitaji unaweza kuyapata kwenye vitabu.
2. Hukuwezesha kufikiri kwa kina
Kwa hakika vitabu huongeza sana uwezo wa kufikiri. Unaposoma vitabu unafahamu mambo ambayo yatakufanya ufikiri zaidi; mara nyingine kitabu kitakuacha na maswali ambayo yatakufanya utafakari kwa kina zaidi juu ya mambo mbalimbali.
3. Hukuongezea uwezo wa lugha
Mbinu moja wapo ya kuongeza uwezo wa lugha ni kusoma machapisho mbalimbali yaliyoandikwa kwa lugha unayotaka kujifunza.
Kwa kusoma vitabu utaongeza msamiati, utajifunza sarufi ya lugha au hata mbinu mbalimbali za matumizi ya lugha.
Unachotakiwa kuzingatia hapa ni kusoma vitabu bora mara nyingi kadri uwezavyo.
Soma pia: Mbinu 10 za Uhakika za Kufahamu Kiingereza/English kwa Muda Mfupi
4. Hukuburudisha
Vitabu ni burudani ya kipekee na ya gharama rahisi unayoweza kutembea nayo mahali popote. Viko vitabu mbalimbali tena vya bei rahisi ambavyo vinaweza kukuburudisha na kukufurahisha.
Vitabu hasa vile vya kifasihi ni burudani tosha ya aina yake. Unaweza kusoma vitabu vilivyochapishwa au vitabu pepe kwa kutumia simu au kompyuta yako.
5. Hukupa hamasa
Maisha yana changamoto mbalimbali; hivyo utahitaji kitu cha kukuhamasisha kutoka hatua moja hadi nyingine. Kwa kusoma vitabu vya hamasa kuhusu maswala mbalimbali ya maisha utaweza kuhamasika zaidi.
Vipo vitabu vilivyoandikwa kukuhamasisha au vilivyo andika maelezo ya watu waliofanikiwa na jinsi walivyopita kutoka  changamoto moja hadi nyingine.
6. Hukuokolea pesa
Vitabu havihitaji umeme, mafuta au matengenezo ili kufanya kazi. Baadhi ya vitabu vingine pia hufundisha mbinu mbalimbali za kuokoa pesa.
Hali kadhalika kusoma vitabu kutakuokolea pesa nyingi ambazo ungezitumia kwenye maswala kama vile starehe.
Soma pia: Njia 10 Zitakazokuwezesha Kutumia Pesa Vyema
7. Hukuwezesha kutumia muda vizuri
Unapotumia muda wako kusoma vitabu, ni wazi kuwa hutopata muda wa kupoteza. Kusoma vitabu kutakufanya utumie muda wako kuongeza maarifa yako zaidi.
Soma pia: Kanuni 9 za Kufanikiwa katika Matumizi ya Muda
8. Huongeza uwezo wa uandishi
Huwezi kuwa mwandishi bora kama husomi vitabu vya waandishi wengine bora.
Ni lazima ujifunze namna waandishi wengine wanavyopanga mawazo, wanavyotumia lugha pamoja na mbinu nyingine za kiuandishi.
Soma pia: Mbinu 7 za Kuwa Mwandishi Bora
9. Huboresha afya yako
Vipo vitabu vingi vinavyotoa maarifa juu ya kuboresha afya yako. Kwa kusoma vitabu hivi utapata maarifa juu ya mambo unayoweza kufanya ili afya yako iwe salama na bora zaidi.
10. Hukuwezesha kujenga hoja
“Fikiri kabla ya kuzungumza. Soma kabla ya kufikiri.”
Ni ukweli usiopingika kuwa Fran Lebowitz alifahamu wazi kuwa huwezi kuzungumza kabla ya kufikiri na huwezi kufikiri kabla ya kusoma. Kusoma kunakupa uwezo wa kufikiri na kujenga hoja zenye nguvu.
Ikiwa unataka kuzungumza ili watu wakuamini na wakusikilize, basi soma vitabu kila mara.
11. Hukuongezea kipato
Waandishi mbalimbali wa vitabu wamekuwa wakiwafundisha wasomaji wao njia za kuongeza kipato chao. Vipo vitabu vinavyofundisha juu ya mikakati ya uwekezaji pamoja na mbinu mbalimbali za kuongeza kipato.
Ukitaka kuongeza kipato ni lazima uongeze pia kiwango chako cha kusoma vitabu.
12. Hukuongezea ubunifu
Tofauti kubwa iliyopo kati ya kusoma vitabu na kuangalia televisheni ni juu ya kuongeza ubunifu wako.
Kadri unavyosoma vitabu, ndivyo unavyojifunza mambo mapya zaidi ambayo yatakufanya kuwa mbunifu.
Kwa kusoma vitabu pia unaweza kufahamu jinsi watu wengine walivyotumia ubunifu kutimiza malengo yao pamoja na kukabili changamoto mbalimbali.
13. Huondoa msongo wa mawazo
Kusoma vitabu hukufanya uondoke katika lindi kubwa la mawazo yanayokutesa na kukutafakarisha juu ya mambo mengine. Waandishi wa vitabu hujenga mazingira ambayo msomaji hujihisi yumo ndani yake.
Hivyo kwa kusoma vitabu, utaliwazwa, utafarijiwa na hata kutiwa moyo huku ukihamishwa katika mawazo yanayokutesa
14. Hukuwezesha kuacha tabia mbaya
Kwa njia ya kusoma vitabu unaweza kujifunza mbinu mbalimbali za kuacha tabia kama vile ulevi, uvivu, uzinzi, sigara, n.k.
Pia kwa kusoma vitabu utatumia muda vyema na kukosa muda wa kutekeleza tabia mbaya.
Soma pia: Mbinu 9 za Kuacha Tabia Mbaya
15. Hukuongezea uwezo wa kumbukumbu
Kadri unavyosoma vitabu ndivyo unavyoongeza uwezo wako wa kumbukumbu. Kwani kila mara unaongeza mambo mapya ambayo unatakiwa kuyakumbuka.
Jinsi ubongo unavyopokea mambo mapya ndivyo unavyozidi kuongeza uwezo wake zaidi
Hitimisho
Naamini sasa unakubaliana na mimi kuwa kuna vito vya thamani sana vilivyofichwa kwenye vitabu ambayo watu wengi hawavifahamu.
Ni muhimu ukajijengea utamaduni wa kusoma vitabu mara kwa mara kadri uwezavyo. Unaweza kutumia programu kama vile Balabolka ili kubadili vitabu kuwa sauti na uvisikilize badala ya kuvisoma.
Soma pia: Balabolka: Programu Inayobadili Maandishi au Vitabu Kuwa Sauti
Je wewe huwa unasoma vitabu? Je unapata manufaa gani? Tafadhali andika maoni yako hapo chini kisha washirikishe wengine makala hii.
Kornelio ni mjasiriamali, mfuasi mkubwa wa masuala ya kompyuta na msanifu mtandao toka mwaka 2008. Amekuwa akifanya kazi mbalimbali zinazohusiana na Teknolojia ya Habari Mawasiliano (TEHAMA), bila kusahau uandishi wa makala kadha wa kadha katika tovuti na blog mbalimbali. Anapenda kujifunza na kuwafundisha watu wengine mambo mbalimbali pamoja na mbinu za kuboresha maisha ya kila siku.
nimeipenda makala hii kwani inamabadiliko kwa baadhi ya watu wanaoelewa ni kipi kinachozungumziwa hivyo hata mimi pia napenda kuandika makala kama hizi hasa zile za kuhamasisha(motivate) watu, kwaiyo nimeipenda
Asante sana Ndugu Rajabu; nafurahi kusikia umeifurahia makala hii; pia nafurahi na nashukuru kwa kutoa maoni yako mazuri. Ni kweli watu wanaopenda maarifa wakisoma makala hii watajifunza kitu. Hongera kwa kuwa pia unapenda kuandika makala za kuhamasisha wengine. Unakaribishwa kuandika makala kwenye tovuti hii pia; unaweza kusoma maelezo hapa (https://www.fahamuhili.com/andika-makala/). Asante na karibu sana.
ningependa kujua faida za mawasiliano ya maandishi ni aina zipi?
Nashukuru kwa kusoma makala za Fahamuhili.com pamoja na kutoa maoni yako. Faida za mawasiliano ya maandishi ni hizi zifuatazo.
1. Mawasiliano ya maandishi ni rahisi kuhifadhiwa
2. Mawasiliano ya maandishi hayapotezi ubora
3. Huonyesha mamlaka (taarifa za mdomo huonekana duni tu)
4. Huweza kutumiwa kama marejeo (Reference)
5. Hudumu kwa muda mrefu zaidi
6. Ni mawasiliano yenye uwezo wa kudhibitishwa
7. Hayatoi mwanya wa kuvurugwa au kubadilshwa kirahisi
8. Huwasilishwa kama yalivyo/yalivyokusudiwa au kwa usahihi
Asante.
Tunafaidika sana na post zako kitaaluma.. Ahsante sana ndugu ndugu mwandishi na mhariri kwa ustadi wa kiwango cha juu
Asante sana kwa maoni yako mazuri na yenye kutia moyo; karibu sana Fahamuhili.com
Ndugu yangu leo nimepitia hapa na nimepata nukuu za kuniwezesha kuwajenga vijana kiakili….barikiwa sana
Nashukuru sana na nimefarijika sana Bro Willy kwa kuona maoni yako; asante kwa kunijuza kuwa Fahamuhili imekufaa kwa namna moja au nyingine. Asante na karibu tena Fahamuhili.com
Ukweli nimepata hamasa kubwa kupitia fahamu hili maana nilihisi huvimbe akilini kutojua mimi nina na nilizaliwa kwasababu gani ? maana ukweli sikujiona mimi wamaana nilikua mtu wa mitandao ya kijamii nikitoka kazi tu naingia mitandaoni kweli Brother Mungu akubariki.
Asante sana kwa maoni yako ya thamani, ni furaha kuwa makala zetu zimekuwa za manufaa kwako; karibu sana Fahamuhili.com
Ni sahihi mafundisho mazuri.
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; na kwa kuwa msomaji wetu. Karibu sana Fahamuhili.com