Njia 12 za Kupunguza Gharama za Uendeshaji wa Kampuni - Fahamu Hili
Tuesday, October 3Maarifa Bila Kikomo
Shadow

Njia 12 za Kupunguza Gharama za Uendeshaji wa Kampuni

Washirikishe Wengine Makala Hii:

Kupunguza gharama

Mbinu mojawapo ya kuongeza faida katika kampuni au biashara yako ni kwa kupunguza matumizi ya kampuni yako. Suala la kupunguza matumizi ya pesa ni muhimu zaidi hasa pale ambapo kampuni inakuwa inakabiliwa na changamoto za kifedha.

Kwa hakika kupunguza matumizi ya uendeshaji wa kampuni ni jambo linalowezekana ikiwa mikakati na hatua stahiki zitachukuliwa.

Ikiwa unapenda kufahamu jinsi ya kupunguza gharama za uendeshaji wa kampuni, basi fahamu njia 12 unazoweza kuzitumia kufanikisha lengo hili.

1. Tathimini upya matumizi

Kuna matumizi mbalimbali kwenye kila kampuni lakini siyo yote ni ya muhimu. Matumizi mengine ni ya lazima lakini yamepewa kipaumbele kuliko umuhimu wake.

Kwa kupunguza matumizi ya vitu kama vile simu, umeme, maji, mafuta au hata intaneti, kutaokoa kiasi kikubwa cha pesa.

Hakikisha huduma hizi zinatumiwa vyema tena kwa matumizi ya muhimu ya kampuni na si vinginevyo.

Soma pia: Njia 8 za Kuokoa Mafuta Unapoendesha Gari

2. Punguza gharama za uzalishaji

Uzalishaji wa bidhaa au utoaji wa huduma hugharimu pesa. Hata hivyo kuna mambo unayoweza kuyafanya ili kupunguza gharama za uzalishaji.

Kwa mfano kama unatumia vifungashio vya bidhaa vya bei kubwa, basi tumia vifungashio mbadala vya bei nafuu.

Inawezekana pia unatumia nishati ya umeme kufanya kila kitu, unaweza kutumia nishati mbadala kama vile umeme jua (solar) au gesi.

3. Ongeza matumizi ya teknolojia

Teknolojia ni muhimu sana kwa ajili ya kupunguza gharama za uendeshaji wa kampuni pamoja na kurahisisha utendaji kazi wa kampuni.

Ikiwa kampuni yako inatumia mawasiliano ya posta, fax, vikao vya kawaida pamoja na utunzaji wa kumbukumbu kwa njia ya karatasi, sasa ni wakati wa kuacha mifumo hiyo.

Matumizi ya barua pepe (email), mikutano kwa njia ya mtandao (online meetings), hazina pepe (cloud storages) kutapuguza gharama kubwa za uendeshaji wa kampuni.

4. Ajiri kupitia mtandao wa intaneti

Hivi leo kampuni nyingi huajiri wafanyakazi kwenye mtandao kwa lengo kubwa la kupunguza gharama za wafanyakazi.

Unapoajiri mtu kwenye mtandao, utamlipa malipo ya kazi husika pekee, lakini unapoajiri mtu moja kwa moja ofisini kwako utamlipa gharama mbalimbali kama vile mafao, bima, gharama za uhamisho, malipo ya likizo, n.k.

Unaweza kutumia tovuti mbalimbali kuajiri wafanyakazi kote duniani kadri upendavyo. Kwa mfano unaweza kutumia tovuti kama vile Upwork na Fiverr.

5. Uza vitu vya zamani

Je kampuni yako ina samani, vyombo, mashine, magari, au hata vifaa vya kielektroniki kama vile kompyuta za zamani?

Badala ya kuweka vifaa hivi viharibikie ghalani (store), unaweza kuviuza kama vifaa chakavu kwa bei nafuu na ukapata pesa ambazo zingepunguza gharama za uendeshaji wa kampuni yako.

6. Tafuta watoa huduma wa bei nafuu

Kuna watoa huduma tofauti na wenye gharama tofauti pia. Ili kupunguza gharama za uendeshaji wa kampuni unaweza kutafuta watoa huduma kama zile za simu, mtandao au hata wale wanaokuletea bidhaa mbalimbali ambao gharama zao ni nafuu.

7. Fanya biashara kwenye mtandao

Biashara kwa njia ya mtandao inaweza kuzalisha faida kubwa na kupunguza kiasi kikubwa cha gharama za uendeshaji wa kampuni ikiwa itafanywa jinsi ipasavyo.

Kwa kutumia tovuti, blog au mitandao ya kijamii unaweza kujitangaza na kuwafikia wateja wengi kwa urahisi zaidi kuliko njia ya kawaida.

Soma pia: Makosa 8 ya Kuepuka Unapofanya Biashara Kwenye Mtandao

8. Nunua vitu kwa ujumla

Kila mfanya biashara anafahamu wazi kuwa kununua vitu kidogokidogo ni hasara zaidi kwani kodi huwa kubwa na punguzo huwa dogo.

Ili kupunguza gharama za uendeshaji wa kampuni, ni muhimu kuzingatia kununua vitu kwa ujumla kuliko rejareja.

9. Tumia njia mbadala za matangazo

Zipo njia nyingi za kutangaza kampuni au biashara yako. Baadhi ya njia ni za gharama kubwa wakati nyingine ni rahisi na za bei nafuu.

Unaweza kutumia mitandao ya kijamii, tovuti, blog au hata vipeperushi ili kujitangaza; kwa njia hii utapunguza gharama za matangazo ya televisheni au redio.

Soma pia: Njia 9 za Kutangaza Biashara Yako Bila Pesa

10. Lipa madeni kwa wakati

Unapochelewa kulipa deni, hasa deni la taasisi za kifedha, husababisha riba kuongezeka. Jambo hili litakusababishia gharama na matumizi makubwa kwenye kampuni yako.

Ikiwa unatumia mikopo kuendesha kampuni yako, hakikisha mikopo hiyo inalipwa kwa wakati.

Soma pia: Sababu 13 za Kwa Nini Biashara Nyingi Hufa

11. Ruhusu likizo zisizokuwa na malipo

Likizo zisizokuwa na malipo hazimpi tu mfanyakazi faida ya kuwa na muda mrefu wa kutosha wa likizo, bali zinanufaisha pia kampuni kwa kuipunguzia gharama za malipo ya likizo.

Ikiwa kampuni yako haitopata shida kutoa muda mrefu wa likizo kwa wafanyakazi usiokuwa na malipo, basi ruhusu wafanyakazi waweze kuomba likizo za aina hii.

12. Punguza wafanyakazi

Njia hii siyo nzuri hasa kwenye maisha ya wafanyakazi, lakini wakati mwingine inabidi kutekelezwa.

Ikiwa kuna wafanyakazi ambao siyo lazima kuwa nao, au ambao majukumu yao yanaweza kufanywa na wafanyakazi wengine, basi wanaweza kupunguzwa ili kupunguza gharama za uendeshaji wa kampuni.

Hitimisho

Kwa hakika matumizi mazuri ya pesa pamoja na mipango endelevu ni mikakati muhimu itakayowezesha kupunguza gharama za uendeshaji kwa kiasi kikubwa. Ni muhimu kuhakikisha pesa zote zinazoingia kwenye matumizi ya kampuni zinaleta faida kwa kampuni husika.

Je una swali au maoni yoyote? Tafadhali tuandikie maoni yako hapo chini kisha washirikishe wengine makala hii. Unaweza kujiunga nasi kwa barua pepe au kwa kulike ukurasa wetu wa Facebook ili kufahamu mengi zaidi.

2 5 votes
Pendekeza Ubora wa Makala Hii
Washirikishe Wengine Makala Hii:
Subscribe
Notify of
guest

3 Maoni
Oldest
Newest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Abdallah mussa
Abdallah mussa
3 years ago

Naitwa abdallah mussa nataka kuanzisha biashara Ila watu ambao nawaomba ushauri wananivunja moyo ndomana nimeamua kutumia mtandao kupata msaada.

Kweba
Kweba
1 year ago

Vitu vipi vya kuzingatia katika uendeshaji kampuni

3
0
Would love your thoughts, please comment.x
()
x