Watu wengi wanakabiliwa na kuathiriwa na hofu katika maisha yao kwa namna moja au nyingine. Hofu hizi zinaweza kusababishwa na mazingira, mtu, kitu au hata sababu za kisaikolojia.
Hofu isiposhughulikiwa kwenye maisha inaweza kuwa ni kikwazo kikubwa cha mafanikio ya mtu husika. Wengi wanatamani kukabiliana na hofu lakini bado hawajui namna ya kukabili hofu zinazowakumba.
Soma pia: Aina 70 za Hofu (Phobia) Unazotakiwa Kuzifahamu.
Je uko tayari kushinda hofu sasa? Karibu nikushirikishe njia 7 ambazo unaweza kuzitumia kukabiliana na hofu maishani mwako.
1. Punguza au ondoa mawazo na imani potofu
Wakati mwingine watu wanapata hofu kutokana na imani au fikra potofu pekee. Kwa mfano unaogopa kinyonga kwa sababu umesikia kuwa kikikugusa utatokwa na ngozi au kufa; je una uhakika juu ya swala hili?
Maswala mengi yanayowaogopesha watu ni kutokana na imani potofu tu na wala hakuna ukweli wowote. Chunguza kama kweli swala linalokupa hofu ni la kweli au ni fikra na imani potofu tu.
2. Kizoee kile kiachokupa hofu
Kukikimbia kile kinachokuogopesha hakuwi suluhisho la hofu yako bali huifanya iimarike zaidi. Kwa mfano ikiwa unaogopa mbwa, basi ukimwona mbwa usikimbie; kaa na jitahidi kumzoea.
Kwa njia hii baada ya muda utaweza kukizoea kile kinachokutisha na hutokuwa na hofu tena unapokutana nacho.
3. Tafakari madhara ya hofu
Hebu fikiri jinsi hofu itakavyoathiri ufanisi na utendaji kazi wako; usikubali hofu ionekane kubwa kuliko madhara yake.
Kama hofu hutuzuia kufanya kazi vizuri na kwa ufanisi ule unaotakiwa, kwanini itutawale? Kwa mfano ikiwa una hofu ya mitihani; umeshawahi kufikiri jinsi hofu hiyo itakavyokuathiri katika mitihani yako kuliko hata kilichokuwa kinakutisha kwenye mitihani yenyewe?
Fikiri tofauti sasa, usikubali hofu ikutawale kuliko athari zake. Ukizingatia hili hutoogopa tena hofu bali utaiepuka kwani hutokubali iathiri kile unachokifanya.
4. Usijaribu kuwa mkamilifu
Kila mtu ana mapungufu yake, hivyo kuogopa kwa ajili ya udhaifu fulani au kujitahidi kuepuka hofu ili uwe mkamilifu ni makosa.
Tambua udhaifu wako na ukubali ili uweze kukabiliana nao. Epuka kuhofu mambo ambayo hayana sababu. Tambua kila mtu ana udhaifu wake; tofauti yetu ni namna tunavyokabiliana na udhaifu huo pekee.
Soma pia: Mambo 25 Unayoweza Kujifunza Kutokana na Makosa.
5. Kumbuka mambo au maeneo ya furaha
Njia nynginne ya kukabiliana na hofu ni kujikumbusha mambo au maeneo ya furaha. Mara unapopatwa na hofu jikumbushe eneo au jambo ambalo huwa linakupa furaha na ujasiri.
Kumbuka, “tunavyofikiri ndivyo tunavyokuwa”. Hebu jitahidi kutafakari jinsi lile eneo au jambo lingine linavyokupa furaha na amani kuliko hata hilo dogo linalokupa hofu.
Fikiri pia jinsi ulivyokutana na mambo mengine yaliyokupa hofu kwenye maisha yako lakini yakapita bila tatizo lolote; hivyo usikubali hofu yoyote kutawala fikra zako.
6. Tumia njia za asili
Katika kupambana na hofu, kamwe usitumie dawa au kilevi cha aina yoyote. Hofu ni swala la asili na la kisaikolojia zaidi.
Matumizi ya vitu kama pombe ili kukabiliana na hofu vinaweza kukuathiri zaidi kuliko kukusaidia.
Kwa mfano hebu fikiri unahofu ya kuzungumza mbele za watu, kisha unakunywa pombe ili upate ujasiri; moja kwa moja unaweza kufanya vituko au kuwa jasiri kupita kiasi mbele za watu na ukajiaibisha zaidi.
Kwa mfano pia, kama una hofu unapokuwa mwenyewe nyumbani, unaweza kufungua redio au televisheni ili nyumbani pasiwe kimya sana.
Ni hakika kama utazingatia njia za asili za kukabili hofu utaweza kupata matokeo mazuri zaidi.
7. Zungumza na omba ushauri
Hakuna tatizo jipya duniani; hofu inayokukabili wewe ilishawakabili watu wengi na wakafanikiwa kuishinda. Hivyo omba ushauri na zungumza na mtu sahihi ili akusaidie kukabiliana na hofu yako.
Uliza njia ambazo watu wengine wanazitumia kukabili hofu kama yako; kumbuka kuwa kuzungumza kile kilichoko katika fikra na moyo wako ni tiba kubwa sana itakayokuwezesha kukabili hofu.
Hitimisho
Ni wazi kuwa hofu inasumbua na kutesa watu wengi katika maisha yao kutokana na kutokufahamu njia za kuikabili. Naamini baada ya kusoma makala hii umebainisha wazi njia unazoweza kuzitumia ili kukabiliana au kushinda hofu.
Usikubali hofu ididimize mafanikio na malengo yako. Je bado una tatizo la hofu? Je wewe unakabili vipi hofu?
Ikiwa una swali au maoni tafadhali usisite kutuandikia hapo chini. Karibu ufuatilie ukurasa wetu wa Facebook ili kufahamu mengi zaidi; pia usisahau kuwashirikisha wengine makala hii.
Kornelio ni mjasiriamali, mfuasi mkubwa wa masuala ya kompyuta na msanifu mtandao toka mwaka 2008. Amekuwa akifanya kazi mbalimbali zinazohusiana na Teknolojia ya Habari Mawasiliano (TEHAMA), bila kusahau uandishi wa makala kadha wa kadha katika tovuti na blog mbalimbali. Anapenda kujifunza na kuwafundisha watu wengine mambo mbalimbali pamoja na mbinu za kuboresha maisha ya kila siku.
Thankx kwa makala yako imenifumbua Sana kutoamini imani potofu
Asante sana. Karibu tena Fahamuhili.com
shukran sana nimepend sana nimambo yako wazi
Asante sana kwa maoni yako ya thamani kwetu; karibu sana Fahamuhili.com
😘 hakika nmejifunz kupitia njia hzi shukrn sana napenda niendelee kujifunz zaid ya hap
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; karibu sana Fahamuhili.com
kiukweli nimependa maoni yenu ningependa kujifunza zaid
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; na kwa kuwa msomaji wetu. Karibu sana Fahamuhili.com
Asante sana kwa ushauri ila hofu inayonikabili ipo kwenye mazingira Nikienda popote mfano hosptal hadi presha inapanda msaada please
Pole kwa tatizo lako Bety; tafadhali fanyia kazi makala yetu. asnate na karibu Fahamuhili.com
Kama umefeli na bado mitihan mengne unaendelea unawezaje ukaitoa hio hofu maana imekua ikinisumbua sana
Mimi ninahofu inanisumbua mno nikitembea najihic kama nataka kudondoka mda mwingine naogopa hata kutembea hata kaz zangu sifanyi kwa ufasaha na kuwa na tetemeka kila nikijalibu kuwa sawa nashindwa plz naomba ushaur
Hofu yangu ni kuongea mbele za watu yaan hii kitu inanitesa sana.
Fanya Mazoezi zaidi. Asante sana kwa maoni yako ya thamani; na kwa kuwa msomaji wetu. Karibu sana Fahamuhili.com
Sante sana nimejifunza kitu kuhusu makala yako Mungu akubariki
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; na kwa kuwa msomaji wetu. Karibu sana Fahamuhili.com