Sio watu wengi wanaopenda au wanafahamu umuhimu wa kuwafundisha watu wengine kile wanachokifahamu. Wengi huona kuwa kufundisha watu wengine ni kazi duni ambayo haiwezi kuwanufaisha kwa njia yoyote ile.
Ukweli ni kuwa kufundisha watu wengine ni swala lenye manufaa mengi ambayo watu wasiofanya hivyo wanayakosa. Ikiwa unapenda kuwa bora zaidi pamoja na kuongeza maarifa yako, basi karibu nikufahamishe faida 6 za kufundisha watu wengine.
1. Hukuongezea maarifa
“Mwalimu ni mwanafunzi wa kudumu.”
Kufundisha wengine ni njia bora ya kuongeza maarifa yako. Kwanza kabisa utahitajika kujiandaa kwa kusoma na kujifunza mambo mbalimbali ili uweze kufundisha vyema, hili litakuongezea kiwango kikubwa cha maarifa.
Pili wakati wa kufundisha utajifunza mambo mbalimbali kutoka kwa yule unayemfundisha au wale unaowafundisha kwani nao kuna mambo wanayoyafahamu tofauti na wewe.
Soma pia: Faida 15 za Kusoma Vitabu Unazotakiwa Kuzifahamu
2. Hukufundisha kupanga na kuandaa
Ili uweze kufundisha vyema ni lazima upangilie na kuandaa kile utakachofundisha. Kwa njia hii utajifunza kupanga na kuandalia somo au mada yako kabla ya kuiwasilisha.
3. Buboresha uwezo wako wa mawasiliano
Utahitaji kuwasiliana na wale unaowafundisha ili wapate kile unacholenga kuwafundisha. Kwa njia hii utaboresha uwezo wako wa kuwasiliana.
Hili linahusisha pia kuboresha uwezo wako wa uandishi pamoja na uwezo wa kuzungumza mbele za watu ikiwa utakuwa unafundisha ana kwa ana.
Soma pia: Njia 10 za Kujenga Uwezo wa Kuzungumza Mbele ya Watu
4. Huwezesha kujitathimini
Njia bora ya kujitathimini ni kwa kufundisha watu wengine kile unachokijua kisha uwaruhusu wakupe tathimini ya uwezo wako.
Kwa njia hii utatambua ni jambo gani unalolifanya kwa ubora na ni wapi unapofanya kwa udhaifu ili ufanye maboresho zaidi.
5. Hukuwezesha kutatua matatizo ya watu
Kuwafundisha watu mambo mbalimbali ni njia bora na ya gharama nafuu ya kutatua matatizo yao. Hebu fikiri unamfundisha mtu jinsi ya kujikinga au kutibu maradhi fulani, akifanyia kazi maarifa hayo na kuona matokeo tayari utakuwa umetatua tatizo lake.
Kwa mfano pia unaweza kumfundisha mtu jinsi ya kujikwamua kiuchumi na akatoka kwenye matatizo ya kifedha; kwa njia hii utakuwa umefanya jambo kubwa kuliko hata kumpa pesa.
6. Hukutengenezea kumbukumbu muhimu
Ni vigumu sana kwa mwanafunzi kumsahau yule aliyemfundisha. Hili hujenga mahusiano na kumbukumbu nzuri kati yako na yule uliyemfundisha.
Huwezi kufahamu kesho utamkuta wapi yule uliyemfundisha na atakusaidia kwa njia gani. Hivyo kufundisha wengine hujenga kumbukumbu nzuri na ya kipekee.
Neno la mwisho
Kwa hakika huwezi kufahamu umuhimu au faida za kufundisha wengine ikiwa hujaanza kufundisha bado. Mimi mwenyewe awali nilikuwa nawaza kuwa nina mambo machache sana ya kuwafudhisha wengine, lakini baada ya kuyaweka kwenye mpangilio mzuri nimeona yakipokelewa vizuri sana na kuleta matokeo mazuri.
Hivyo ikiwa una maarifa fulani basi usisite kuyatoa kwa wengine ili wote mnufaike. Unaweza kufundisha kupitia mitandao ya kijamii, blog au hata ana kwa ana.
Je wewe huwa unafundisha wengine kwa njia moja au nyingine? Je unanufaikaje?
Kornelio ni mjasiriamali, mfuasi mkubwa wa masuala ya kompyuta na msanifu mtandao toka mwaka 2008. Amekuwa akifanya kazi mbalimbali zinazohusiana na Teknolojia ya Habari Mawasiliano (TEHAMA), bila kusahau uandishi wa makala kadha wa kadha katika tovuti na blog mbalimbali. Anapenda kujifunza na kuwafundisha watu wengine mambo mbalimbali pamoja na mbinu za kuboresha maisha ya kila siku.
Ni vyema kabisa mngetuwekea vitabu maan masomo yenu ni mazuri sana.
Nashukuru sana kwa kutembelea blog yetu ya Fahamuhili; tunashukuru pia kwa maoni yako mazuri. Naahidi kufanyia kazi pendekezo lako.
asant sana kwa makala nzuri
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; karibu sana Fahamuhili.com