Google ni rafiki wa karibu katika maisha yetu. Kupitia injini pekuzi ya Google tunaweza kupata majibu ya maswali mbalimbali. Ni ukweli usiopingika kuwa katika matumizi yetu ya teknolojia hatuwezi kuepuka kutumia Google.
Kupitia Google unaweza kupata majibu ya maswali mbalimbali, kazi, marafiki, bidhaa, huduma, elimu n.k.
Pamoja na nafasi hii kubwa ya Google kwenye maisha na kazi zetu, bado watu wengi hawafahamu vyema matumizi mbalimbali ya Google.
Karibu nikufahamishe mambo 10 usiyojua kama unaweza kuyafanya kwa kutumia Google.
1. Kikokotozi (calculator)
Ikiwa unataka kufanya mahesabu kadhaa, huhitaji kikokotozi au simu yenye kikokotozi kama uko karibu na Google. Kwa kuandika neno calculator kwenye ukurasa wa Google mara moja utapata kikokotozi kwa ajili ya kufanyia hesabu.
2. Kufahamu muda wa jua kuchomoza na kuzama
Kupitia Google unaweza kutazama muda wa kuchomoza na kuzama kwa jua kwenye eneo fulani.
Kwa mfano unaweza kuandika “sunrise Nairobi” au “Sunset Dar es Salaam” kwenye Google na utapata muda wa jua kuchomoza au kuzama kwenye mji husika.
3. Viwango vya kubadilisha fedha
Je umekuwa ukipata shida kufahamu viwango vya kubadilisha fedha mbalimbali duniani?
Usihangaike tena, unaweza kuandika “currency convertor” kwenye Google na mara moja utapata ukurasa kwa ajili ya kufahamu viwango vya kubadilishia fedha.
4. Maana za maneno
Je unasumbuka kubeba kamusi ya Kiingereza kila unapokuwa? Ukiwa na Google huhitaji kubeba kamusi kwani unaweza kupata maana za maneno yote kupitia Google. Unachotakiwa kufanya ni kuandika “Dictionary” kwenye Google kisha utapata dictionary unayoweza kuitumia kutafuta maneno mbalimbali. Unaweza pia kuandika “define your_word” na utapata maana ya neno uliloliandika.
5. Tafsiri
Unaweza kutafsiri maneno kutoka lugha moja hadi nyingine kwa urahisi na bure kabisa uwapo na Google.
Unaweza pia kusoma maandishi kwa sauti kupitia Google; kwa mfano ikiwa unataka kusikiliza andiko fulani badala ya kulisoma basi unaweza kutumia Google translate.
Unachotakiwa kufanya ni kutafuta “translate” kwenye Google kisha utapata ukurasa unaoweza kuweka maandishi yako pamoja na kuchagua lugha.
6. Kubadilisha vipimo
Je huwa unahitaji kubadili vipimo mbalimbali? Unaweza kubadili vipimo mbalimbali kwa kutumia Google. Kwa kutafuta “unit converter” utapata ukurasa wenye kukuwezesha kubadilisha vipimo mbalimbali.
7. Kihesabu muda
Unaweza kupata kihesabu muda (timer and stopwatch) kizuri kitakachokusaidia katika shughuli mbalimbali kwa kutumia Google. Unachotakiwa kufanya ni kutafuta neno “timer” kisha uweke muda unaotaka kuhesabu na ubonyeze start.
8. Hali ya hewa
Hakuna haja ya kukaa kusubiri tena habari za hali ya hewa. Kwa kutumia Google, unaweza kufahamu hali ya hewa ya miji na maeneo mbalimbali duniani.
Kwa mfano unaweza kutafuta “Weather Kampala” au “Weather Arusha” na utapata taarifa kamili.
9. Kufahamu kurasa za tovuti fulani zilizoko kwenye Google
Ikiwa unataka kufahamu ni kurasa ngapi na zipi zimeorodheshwa au kutambulika (indexed) na Google katika tovuti fulani, unaweza kuandika “site:mfano.com” na utaona kurasa za tovuti yako.
Huduma hii ya Google ni muhimu sana kwa wenye tovuti na blogs kwani wataitumia kubaini ni kurasa zipi ambazo tayari Google imeshazitambua kutoka kwenye tovuti au blog zao.
10. Kucheza michezo mbalimbali
Kupitia Google unaweza pia kucheza michezo mbalimbali ili kujiburudisha. Kwa mfano ukitafuta neno “zerg rush” kwenye Google utaweza kucheza mchezo wa zerg rush.
Hitimisho
Naamini sasa umekubaliana na mimi kuwa Google ni rafiki yetu bora na wa karibu sana. Ni wazi kuwa yapo mambo mengi sana unayoweza kuyafanya kwa kutumia Google, lakini mimi nimeorodhesha 10 tu. Je wewe huwa unatumia Google kwa mambo haya? Je kuna mambo mengine ambayo wewe unayafanya kwenye Google?
Soma pia: Tovuti 20 Ambazo Ungetamani Kuzijua Mapema.
Tafadhali tuandikie maoni yako hapo chini. Usisahau kuwashirikisha wengine makala hii pamoja na kujiunga na ukurasa wetu wa Fecebook ili kufahamu mengi zaidi.
Kornelio ni mjasiriamali, mfuasi mkubwa wa masuala ya kompyuta na msanifu mtandao toka mwaka 2008. Amekuwa akifanya kazi mbalimbali zinazohusiana na Teknolojia ya Habari Mawasiliano (TEHAMA), bila kusahau uandishi wa makala kadha wa kadha katika tovuti na blog mbalimbali. Anapenda kujifunza na kuwafundisha watu wengine mambo mbalimbali pamoja na mbinu za kuboresha maisha ya kila siku.