Shughuli nyingi pamoja na kubadilika kwa mtindo wa maisha kumewafanya madereva wengi kusinzia wakati wanaendesha magari. Kusinzia wakati wa kuendesha gari kunaweza kusababisha madhara makubwa. Inashauriwa kuwa unapojisikia kuchoka ni vyema ukapumzika.
Panasonic wanaamini kuwa wana utatuzi: kwa kutumia akili bandia (Artificial inteligence) wanaweza kumfanya dereva awe macho wakati wote.
Kwa mujibu wa Panasonic kuna aina tano za kusinzia: kutosinzia, kusinzia kidogo, kusinzia halisi, kusinzia sana na kusinzia kulikopitiliza. Kampuni hii ya Kijapani imegundua mfumo wa kwenye magari unaoweza kutambua kusinzia kwa dereva na kupambana nako kabla ya kutokea.
Mfumo huu humfwatilia dereva kwa kutumia kamera na vihisi (sensors). Mfumo huu unaweza kutambua mambo kama vile kupepesa macho, mkao wa uso na hata hali ya kubadilika kwa joto la mwili. Taarifa hizi hujumuishwa na taarifa za mazingira ya ndani ya gari. Kisha taarifa hizi huchakatwa kwa pamoja kwa kutumia akili bandia (artificila inteligence) ili kubaini kiwango cha kusinzia cha dereva.
Mfumo huu ni bora kiasi cha kubaini kusinzia kwa dereva kabla hata dereva mwenyewe hajahisi kusinzia huko. Hivyo huufanya kuwa rahisi kutengeneza mazingira yatakayomfanya derefa asisinzie.
Kwa kawaida mtu husinzia kutokana na hali ya joto na mwanga hafifu; hivyo mfumo huu hurekebisha hali ya joto na mwanga katika gari ili kumfanya dereva kuwa macho.
Hata hivyo ikiwa dereva anauchovu na usingizi mwingi basi mfumo utabaini na kupiga alamu itakayomlazimisha kupumzika.
Kinachofurahisha katika mfumo huu wa Panasonic ni kuwa hufanya kazi kwa namna ambayo dereva hatambui; yeye hujikuta yuko macho mwanzo hadi mwisho wa safari.
Panasonic wanatarajia mfumo huu utakuwa tayari kwa majaribio kwenye magari mwezi Oktoba. Hivyo kama utapokelewa na watengenezaji wa magari basi utapatikana katika magari yatayozalishwa mwakani.
Je unauonaje mfumo huu? Je unafikiri hili litakuwa ni suluhisho la ajali zinazosababishwa na madereva kusinzia? Tafadhali tuandikie maoni yako kisha washirikishe na wengine.
Kornelio ni mjasiriamali, mfuasi mkubwa wa masuala ya kompyuta na msanifu mtandao toka mwaka 2008. Amekuwa akifanya kazi mbalimbali zinazohusiana na Teknolojia ya Habari Mawasiliano (TEHAMA), bila kusahau uandishi wa makala kadha wa kadha katika tovuti na blog mbalimbali. Anapenda kujifunza na kuwafundisha watu wengine mambo mbalimbali pamoja na mbinu za kuboresha maisha ya kila siku.