Ardhi ni rasilimali muhimu ambayo kila mtu anaihitaji kwa namna moja au nyingine. Watu wengi hununua ardhi kwa ajili ya kufanyia shughuli mbalimbali kama vile ujenzi na kilimo. Pamoja na umuhimu huu mkubwa wa ardhi bado watu wengi wanakumbana na changamoto mbalimbali katika maswala yanayohusu kununua na kumiliki ardhi. Wengi hujikuta wakinyang’anywa ardhi zao, kuharibiwa mali, au wakiingia kwenye migogoro mikubwa ya kisheria.
Ni wazi kuwa zipo sababu mbalimbali zinazosababisha matatizo haya. Fuatilia makala hii kwa makini ili uweze kufahamu mambo 10 ambayo unapaswa kuyazingatia kabla ya kununua kiwanja au ardhi.
1. Ona kiwanja husika mwenyewe
Ni vyema ukafika kwenye eneo la kiwanja husika na kukiona wewe mwenyewe kama kinakuridhisha na kukufaa kwa mahitaji yako. Fahamu mipaka, na vitu vingine vinavyohusu kiwanja kama vile mimea iliyopo, aina ya udongo n.k. Kwa kufanya hivi utaweza kubaini kama kiwanja kinakidhi mahitaji na matumizi yako.
2. Fahamu mmiliki halisi
Matatizo mengi yanayowakumba watu kwenye maswala ya ardhi ni kutokana na kuuziwa ardhi na mtu ambaye si mmiliki halisi wa ardhi. Ni muhimu sana, tena sana, ukamfahamu mmiliki halisi wa ardhi unayotaka kuinunua kabla hujainunua. Kama ardhi imesajiliwa unaweza kwenda wizara ya ardhi ili kufahamu mmiliki halisi.
Pia ni lazima ufahamu kama kiwanja au ardhi kinamilikiwa na wanandoa (matrimonial property) ili upate ridhaa ya familia juu ya kununua kiwanja husika. Mara nyingi watu hasa wanaume huuza viwanja vya familia kwa siri bila kushirikisha familia; jambo ambalo linaweza kukuingiza kwenye mgogoro mkubwa na familia husika. Kwa kumfahamu mmiliki halisi utaweza kuepuka migogoro au kupoteza pesa zako.
3. Epuka madalali
Karibu kila kinachouzwa leo kuna madalali. Madalali hawana cha ziada zaidi ya kutafuta njia za ujanja ujanja za kupata pesa. Kama kiwanja kinauzwa milioni 5 dalali anaweza kukuambia milioni 7 ili apate zake 2. Hivyo ni muhimu kumtafuta mwenye mali halisi ili uzungumze na kupatana naye kuhusu gharama halisi za kiwanja. Kwa kufanya hivi utaokoa pesa zako ambazo zingechukuliwa na madalali.
4. Angalia uwepo wa huduma za kijamii
Uwepo wa huduma za kijamii katika eneo husika ni muhimu sana, lakini watu wengi huwa hawazingatii hili. Ni muhimu kabla hujanunua kiwanja ukaangalia uwepo wa huduma kama vile maji, hospitali, barabara, soko, shule, nyumba za ibada n.k. Hili litakuwezesha hasa kama unataka kuishi eneo husika kupata huduma za kijamii kwa karibu bila shida wala gharama ya ziada.

5. Chunguza migogoro ya kisheria
Kutokana na makosa mbalimbali yanayofanyika kwenye maswala ya ardhi, ardhi nyingi sana hivi leo zina migogoro ya kisheria. Ni vyema ukajiepusha kujitumbukiza kwenye kesi na matatizo yasiyokuwa ya lazima kwa kununua kiwanja au ardhi yenye mgogoro wa kisheria. Unaweza kulibaini hili kwa kufanya uchunguzi wa kina kabla hujanunua ardhi husika.
6. Chunguza kama kiwanja kimewekwa rehani
Viwanja na mashamba huwekwa rehani kwa taasisi mbalimbali hasa zile za kifedha. Watu wenye nia mbaya huuza viwanja vilivyowekwa rehani. Kununua kiwanja hiki kutakuingiza kwenye mgogoro na taassisi husika. Na kwa sababu taasisi hii inakihodhi kisheria, hutoweza kukipata kiwanja husika bali unaweza kupoteza fedha zako.
7. Fahamu hali ya kijografia ya eneo
Nimeshuhudia watu wakiuziwa viwanja kwenye mikondo ya maji pamoja na matindiga; hali inayowapelekea kupata adha kubwa wakati wa mvua. Ni vyema ukafahamu hali ya kijografia ya kiwanja au ardhi unayoinunua. Hakikisha mambo yafuatayo:
- Eneo husika siyo tindiga au kinamasi
- Eneo husika siyo mkondo wa maji – unaweza ukazolewa na mafuriko hapa.
- Eneo husika siyo bonde linalojaa maji
- Eneo husika siyo eneo la magadi
- Siyo eneo la maporomoko ya ardhi
- Siyo eneo lenye ardhi inayotitia n.k

Kwa kutazama baadhi ya mambo kama haya ya msingi, utaweza kuhakikisha unanunua eneo zuri na salama kijografia.
8. Chunguza kama kiwanja kipo kwenye mpago au hifadhi maalumu
Kuna maeneo ya ardhi yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli maalumu. Maeneo hayo yanaweza kuwa ni ya miradi ya serikali, maeneo ya wazi, hifadhi ya barabara, hifadhi ya wanyama pori, chanzo cha maji au hata ardhi ya kampuni au taasisi fulani. Watu wengi wamenyang’anywa ardhi zao au hata pengine kuharibiwa mali zao kwa kosa la kujenga au kufanya shughuli katika maeneo haya.

Inashauriwa kuchunguza ardhi vyema kabla ya kuinunua ili uweze kubaini maswala haya. Pia unaweza kwenda kwenye ofisi zinazoshughulika na maswala ya ardhi na mipango miji ili kupata taarifa kamili.
9. Fahamu kama kuna mpangaji au mkodishaji
Kuna watu wanakodisha ardhi kwa ajili ya shughuli na miradi mbalimbali kwa kipindi fulani cha muda. Hivyo kabla ya kununua ardhi hakikisha kuwa hakuna mkodishaji au mmepatana naye kwanza. Ni vigumu kumtoa mtu aliyekodisha ardhi na kuilipia kwa miaka kumi kwa kigezo tu kuwa umeinunua. Hivyo kuwa makini na chunguza swala hili kabla.
10. Husisha mwanasheria au taratibu za kisheria
Kutokana na ukosefu wa elimu pamoja na hali ya mazoea, watu hujimilikisha ardhi bila kufuata taratibu za kisheria. Ni lazima ufahamu kuwa ardhi ni kitu kinachomilikiwa kisheria. Hivyo ni lazima makabidhiano au manunuzi ya ardhi yazingatie sheria na kuhusisha ushahidi wa kisheria kama inawezekana.
Unapomhusisha mwanasheria katika manunuzi yako ni wazi kuwa utajiwekea uhakika wa kuwa mmiliki halali kwani umefuata taratibu za kisheria. Zipo taasisi nyingi unazoweza kuziona na ukapata usaidizi wa kisheria bure au kwa bei nafuu.
Hitimisho
Naamini umefahamu mambo kumi ambayo ni muhimu sana ukayazingatia kabla ya kununua kiwanja au ardhi. Ni wazi kuwa matatizo na migogoro mingi huibuka kutokana na kutozingatia maswala tajwa hapo juu hasa kutokana na ukosefu wa elimu na kwenda kwa mazoea. Tambua ardhi ni jambo nyeti, usikubali kuzuzuliwa na bei au maneno ya muuzaji; hivyo ni lazima uwe mwangalifu na ufanye uchunguzi wa kina kabla ya kununua kiwanja au ardhi.
Soma pia: Makosa 8 ya Kuepuka Kabla na Wakati wa Kujenga Nyumba.
Je wewe unayazingatia haya kabla ya kununua ardhi? Je ulishapata tatizo la ardhi? Ulilimalizaje? Tafadhali tuandikie maoni yako hapo chini kisha washirikishe wengine makala hii. Unaweza pia kulike ukurasa wetu wa Facebook ili kufahamu mengi zaidi.
Kornelio ni mjasiriamali, mfuasi mkubwa wa masuala ya kompyuta na msanifu mtandao toka mwaka 2008. Amekuwa akifanya kazi mbalimbali zinazohusiana na Teknolojia ya Habari Mawasiliano (TEHAMA), bila kusahau uandishi wa makala kadha wa kadha katika tovuti na blog mbalimbali. Anapenda kujifunza na kuwafundisha watu wengine mambo mbalimbali pamoja na mbinu za kuboresha maisha ya kila siku.
Very nice
Tunashukuru sana. Karibu tena Fahamuhili.com
uko vizuri kijana , Keep it up aisee. Hii website iko very educative
Nashukuru sana Mr. Ray kwa maoni yako mazuri; Karibu sana Fahamuhili.com
Nashukuru sana , umenielimisha . nataka kununua ardhi Kwa elimu hii itanibidi kuwa makini sana zaid ya sasa
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; karibu sana Fahamuhili.com
Kazi nzuri. Ila natamani pia uelezee suluhisho kwa baadhi ya matatizo, maana wasomaji wengi hatuna elimu juu ya ardhi. Mfano, nitajuaje kiwanja kimewekwa rehani, au kimepangishwa…nk. Asante kwa makala hii.
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; Tutafanyia kazi maoni yako. karibu sana Fahamuhili.com
Kazi nzuri sana, jitihada zako ni zenye kuthaminiwa
Tunashukuru sana kwa kuwa msomaji wetu; pia tunashukuru kwa maoni yako ya thamani; tunakutakia kila la heri katika kutimiza malengo yako…karibu sana Fahamuhili.
Asante kwa ushauri mzuri .Kama nataka kununua ardhi ambayo haijapimwa natakiwa nifuate taratibu zipi? Nifanyaje ili nijimilikishe kiwe Mali yangu?
1. Fanya utafiti wa kina
2. Uliza utataribu wa kuuza na kununua ardhi katika eneo hilo kutoka kwa mamlaka za kiserikali zilizoko katika eneo husika.
3. Fanya manunuzi yaliyorasimishwa kisheria ili likitokea tatizo mbeleni upate msaada.
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; karibu sana Fahamuhili.com
Jina langu naitwa Peter Felix Sumbizi . Kwanza nakupongeza Sana , Sana kwa elimu hii ya masuala mazima kuhusiana na mambo ya kuzingatia katika ununuzi wa ardhi ! Ahsante 🙏 Mheshimiwa . Endelea kutuelimisha Watanzania . MUNGU AKUBARIKI SANA !
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; na kwa kuwa msomaji wetu. Karibu sana Fahamuhili.com
Thanks for this
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; karibu sana Fahamuhili.com
Nimeipenda
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; karibu sana Fahamuhili.com
Ni makala nzuri.
Asante sana kwa maoni yako ya thamani; karibu sana Fahamuhili.com
Ahsanteni kwa darasa zuri