
Dunia imeendelea kushuhudia uhaba mkubwa wa rasilimali mbalimbali kutokana na ongezeko kubwa la idadi ya watu.
Moja ya rasilimali ambazo zimekua adimu sana duniani kwa wakati huu ni ardhi, uhaba wa ardhi umefanya wahandisi kote duniani kuumiza vichwa vyao kufikiri namna ambavyo ardhi iliyopo itatumika vyema na kwa manufaa zaidi kwa wengi.
Pamoja na sababu nyingine lukuki, ufinyu wa ardhi umechangia kwa kiasi kikubwa kujengwa kwa majengo marefu na ya kushangaza katika maeneo mbalimbali duniani.
Yafuatayo ni majengo kumi marefu zaidi duniani maarufu kama sky scrapers kwa lugha ya kimombo.
10. International Commerce Centre
Jengo hili linashika nafasi ya kumi kwa majengo marefu zaidi duniani. Lina urefu wa mita 484 pamoja na ghorofa 108; lilijengwa mwaka 2010.
09. Shanghai world financial centre
Jengo hili lina mita za urefu 492 (ghorofa 128), lilijengwa mwaka 2008 katika jiji la tatu kwa wingi wa watu duniani la Shanghai katika jamuhuri ya watu wa China.
08. Taipei 101
Taipei 101 linashika nafasi ya nane kwa urefu wa majengo duniani likiwa na urefu wa mita 509 pamoja na ghorofa 101. Lilijengwa mwaka 2004 na tangu mwaka huo hadi mwaka 2010 lilikua ndiyo jengo refu zaidi duniani kabla rekodi hii haijavunjwa na Burj Khalifa.
Linasifika kwa kuwa jengo kubwa na refu zaidi duniani lenye miundombinu rafiki kwa mazingira (the tallest and largest green building in the World). Linapatikana katika jiji la Taipei nchini Taiwan barani Asia.
07. CTF Finance Centre
Hili linapatikana katika mji wa kiviwanda wa china uitwao Guangzhou. Lina urefu wa mita 509 pamoja na ghorofa 111 na lilijengwa mwaka 2016.
06. One world Trade Centre
Jengo hili linapatikana katika jiji la kibiashara la New York nchini Marekani. Lina urefu wa mita 514 (ghorofa 104) na lilijengwa mwaka 2014.
Jengo hili linafahamika pia kama the “Freedom tower” limejengwa jirani na jengo la World Trade Centre lililoshambuliwa na magaidi September 11 mwaka 2001.
05. Lotte world tower
Linapatikana katika jiji kuu la Korea Kusini la Seoul. Lina urefu wa mita 555 (ghorofa 123) na lilikamilika mwaka 2016.
04. Ping An Finance Centre
Jengo hili lina urefu wa mita 600 (ghorofa 115) na linapatikana katika jiji la Shenzhen China, lilijengwaa mwaka 2016.
03. Abraj AL-Bait clock Tower
Nafasi ya tatu inashikiliwa na jengo hililenye urefu wa mita 601 (ghorofa 120). Linapatikana katika mji mtakatifu kwa Waislamu wa Mecca nchini Saudi Arabia.
Lilijengwa mwaka 2012 na linashikilia rekodi ya kuwa mnara wa saa mrefu zaidi duniani sanjari na kuwa hoteli ndefu zaidi duniani.
02. Shanghai Tower
Jengo hili linapatikana katika jiji la Shanghai China na lina urefu wa mita 632 (ghorofa 128) kutoka uso wa ardhi. Lilijengwa mwaka 2015 na ndilo jengo la pili kwa urefu duniani.
01. Burj Khalifa
Mpenzi msomaji hili ndilo jengo refu zaidi duniani tangu kuumbwa kwa misingi ya ulimwengu. Lina urefu wa mita 829 (ghorofa 163), takribani viwanja nane na nusu vya mpira wa miguu.
Lilikamilika mwaka 2010 na kuvunja rekodi ya Taipei 101. Linapatikana katika jiji la Dubai katika falme za Kiarabu. (UAE)
Soma pia: Mambo 20 Usiyoyajua Kuhusu Jengo Refu Zaidi Duniani la Burj Khalifa.
Fahamu hili! Hong Kong ambayo ni sehemu ya China yenye utawala wake wa ndani ndiyo jiji linaloshikilia rekodi ya dunia ya kuwa na majengo mengi marefu. Ina jumla ya majengo marefu (sky scrapers) 303 idadi ambayo haijafikiwa na jiji lingine lolote duniani.
Chanzo cha picha za majengo ni Wikipedia.
Je una swali au maoni? Tafadhali tuandikie maoni yako hapo chini kisha usisahau kuwashirikisha wengine makala hii. Unaweza pia kufuatilia ukurasa wetu wa Facebook ili kufahamu mengi zaidi.
Kornelio ni mjasiriamali, mfuasi mkubwa wa masuala ya kompyuta na msanifu mtandao toka mwaka 2008. Amekuwa akifanya kazi mbalimbali zinazohusiana na Teknolojia ya Habari Mawasiliano (TEHAMA), bila kusahau uandishi wa makala kadha wa kadha katika tovuti na blog mbalimbali. Anapenda kujifunza na kuwafundisha watu wengine mambo mbalimbali pamoja na mbinu za kuboresha maisha ya kila siku.